Header Ads

Arusha hapakaliki mkuu wa ulinzi na usalama auawa kwa kuchinjwa.....

Arusha. Watu wasiojulikana wamemuua kwa kumchinja Mkuu wa Idara ya Ulinzi na Usalama  katika Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa), Emily Kisamo kisha kumweka katika buti la gari lake.
Tukio hilo lilitokea juzi katika eneo la Lemara nje kidogo ya Jiji la Arusha, huku gari likiwa limetelekezwa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema jana kuwa walipokea taarifa kutoka kwa mke wa marehemu kuwa mumewe tangu aondoke nyumbani siku hiyo asubuhi hakurudi na simu yake ilikuwa haipokewi.

Sabas alisema baada ya kuanza uchunguzi walilikuta gari eneo hilo.
“Tulimwomba mke wa marehemu atuletee funguo za ziada za gari na ndipo tulipofungua tulikuta mwili wa marehemu kwenye buti,” alisema.
Alisema baada ya uchunguzi alikutwa amekatwa na kitu chenye ncha kali shingoni kwa nyuma.
“Bado hatujakamata mtu yeyote aliyehusika na mauaji haya,” alisema.
Habari kutoka ndani ya Tanapa zinaeleza kuwa marehemu alikuwa asafiri kwenda nchini India kwa matibabu.
“Tumepokea kwa mshtuko taarifa za kifo kwani marehemu alikuwa anaumwa na kesho (leo) alikuwa asafiri,” kilisema chanzo cha habari.

Katika utendaji kazi wake, Kisamo atakumbukwa kwa kuwa kinara katika vita dhidi ya ujangili na alikuwa katika kamati za kitaifa za kupambana na ujangili na mara kadhaa alikuwa akitoa elimu juu ya uhifadhi na ulinzi wa wanyamapori.

No comments

Powered by Blogger.