Header Ads

‘Ukomedi’ wamsaidia Kingwendu kuomba kura Jimbo la Kisarawe

Mgombea ubunge wa Jimbo la Kisarawe kupitia Cuf, Rashid Mwinshehe ‘Kingwendu’ juzi alikuwa kivutio wakati akitambulishwa na mgombea mwenza wa urais wa Jamhuri, Juma Duni Haji.

Juma Duni Haji ni mgombea mwenza wa Edward Lowassa anayegombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema, lakini wakiwa chini ya mwamvuli wa vyama vinavyounda Ukawa (Chadema, Nccr-Mageuzi, Cuf na NLD).

Kingwendu ambaye ni msanii wa fani ya uchekeshaji (komedi), alitumia fani hiyo kuomba kura pale alipotambulishwa na mgombea mwenza Juma Duni Haji.


Huku akitumia fani yake ya uchekeshaji, dakika sita alizopewa kuomba kura alizitumia vizuri kwa kuiteka hadhara alipoingiza maneno ya uchekeshaji kwa kusema; “Jamani ndugu zangu ebu niangalieni mie, mbunge nameremeta kwa raha zangu,” alianza hivyo huku macho akiyatoa nje mithili ya mtu aliyepatwa mshtuko wa shoti ya umeme.

“Hebu angalieni jamani yaani wametumwemwenya mwemwenya kama panya tangu uhuru,” alisema huku akiangusha kicheko.

Kila kauli aliyoitoa meza kuu ya mgombea mwenza Juma Duni Haji, ilikuwa ni vicheko tu huku maelfu ya waliofurika viwanjani hapo akimshangilia kwa nguvu na kelele.

“Angalia vijana mtaani wamebadilika kuwa omba omba yaani ukiwapita tu kidogo wanakudakia, oyaaa sasa kaka unatuachaje, tupoze basi braza...yaani tunatembea kwa wasi wasi mtaani,kumbe tatizo ni ajira hakuna na CCM bado wanatuongoza,” alisema na kuongeza:

“Hebu angalia ukitoa na gunia moja tu la mkaa kwenye gari, labda unatoka kusalimia unadakwa na watu wa malia asili unaombwa ushuru, jama mkaa nimepewa zawadi harafu mnaniomba ushuru inakuwaje?.

“Jamani CCM ni sumu kali tena haifai kabisa..., tusifanye makosa kabisa mwaka huu, angalia barabara zimejaa vumbi yaani ukitembea kidogo tu vumbi linakujaa!”

Kilichobadilika kwake ni mavazi tu katika mwonekano wake, lakini bado ni mchekeshaji aliyeamua kutumia nafasi hiyo hiyo kufikisha ujumbe na kujenga hoja za kuishawishi jamii ya wana-Kisarawe kumpigia kura Oktoba 25.

No comments

Powered by Blogger.